Monday, August 29, 2011

Kuelekea Idd Elfitri; TAMSA Mzumbe Watoa Tamko.....Soma Kwa Undani

     Nova Kambota akiwa na Bw Rajab Semgonja Mkuu wa Habari na Mawasiliano TAMSA

Tukiwa tunaelekea sikukuu ya Idd Elfitri baada ya safari ndefu ya siku 30 ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, Blog hii imefanya mahojiano na Tanzania Muslim Students Association(TAMSA) chuo kikuu Mzumbe ambapo Mkuu wa Habari na Mawasiliano wa TAMSA Chuo Kikuu Mzumbe Bw Rajab Semgonja alijibu maswali kadhaa kama ifuatavyo......;


MUSO Link; Baada ya safari ndefu ya siku 30 za kufunga na sasa tukiwa tunahesabu masaa kadhaa kabla ya kusheherekea Idd Elfitri, je una lipi la kusema?

Semgonja; Kwanza shukranzi ziende kwa Mwenyezi Mungu kwa kutuweka salama mpaka hatimaye tumefikia siku hii ambayo tunakaribia kusheherekea siku kuu ya Idd, pia nikiri wazi kuwa muda wote wa Ramadhani umekuwa ni kipindi kizuri kwetu waislamu kujitafakari, kuomba toba, kubadili mwenendo wetu na kumrudia Mwenyezi Mungu mweza wa yote, kwa kifupi ni kipindi ambacho kimetujenga na kutuimarisha kiimani.


MUSO Link; Ikizingatiwa kuwa Mzumbe ni sehemu ya wasomi na zaidi ni vijana pia kuna maswala kama ulevi , uasherati na mengine mengi, je unadhani mwezi wa Ramadhani ulisaidia kupambana na mambo haya kwenye jamii ya Mzumbe?

Semgonja; Ni kweli kabisa ndugu mwandishi kuwa mambo maovu kama hayo yapo, kwa upande mmoja mwezi mtukufu wa Ramadhani umetujenga sana lakini umesaidia baadhi ya watu kubadili mwenendo wao hata hivyo bado hatujafanikiwa kwa asilimia mia moja hivyo mapambano yanaendelea, tutaendelea kuwahimiza wanamzumbe waachane na uovu na kuomba toba kwa Mwenyezi Mungu.


MUSO Link; Kesho ni siku kuu ya Idd , je mmejiandaeje kusherehekea siku hiyo?

Semgonja; Kesho tutakuwa na Baraza la Idd ambapo waislamu tutakusanyika pamoja, kuswali, kupata mawaidha ya walimu,tutasheherekea pamoja na ndugu zetu kutoka Mzumbe secondary na baadhi ya wafanyakazi, sambamba na hayo tutakula pamoja na kupata wasaa mzuri wa kusikiliza nasaha kutoka kwa Maimam na walimu wa Dini yetu, hivyo tunamshukuru Mungu kuwa maandilizi ya siku kuu ya Idd yanaendelea vizuri sana.


MUSO Link; Mwishowe wewe kama kiongozi wa dini na msomi wa chuo kikuu, je nini wito wako kwa waislamu wa Mzumbe na wanamzumbe kwa ujumla?

Semgonja; Kwanza natoa wito kwa waislamu wote kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha siku hii ya Idd lakini pia natoa wito kwa kuwataka Wanamzumbe wote kila mmoja kwa nafasi yake kujitafakari, kutubu , kuwa na mwenendo mwema unaompendeza Mwenyezi Mungu.


MUSO Link; Asante kwa ushirikiano na Idd Mubarak

Semgonja; Asante ndugu mwandishi nasi kama TAMSA tunakukaribisha kwenye Baraza la Idd

No comments:

Post a Comment